Vigogo wa Rahco watumbuliwa jipu Kortini

Posted by Unknown on 13:16 with No comments




Mkurugenzi Mkuu wa zamani wa Kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli Tanzania (Rahco), Benhadard Tito na wenzake wawili wamepadishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, wakikabiliwa na mashtaka manne.
Vigogo wawili wa Rahco na mfanyabiashara wanakabiliwa na mashtaka ya uhujumu uchumi, matumizi mabaya ya madaraka, kula njama na kusababisha hasara ya dola za Marekani 527,540.
Mbali na Tito, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Mwanasheria wa Rahco, Emmanuel Massawe na mfanyabiashara ambaye pia ni mwakilishi wa kampuni ya Rothschild (South Africa) Proprietary Limited, Kanji Mwinyijuma.
Washtakiwa hao watatu walisomewa mashtaka hayo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba, huku upande wa mashtaka ukiwa na Maghela Ndimbo, Janeth Machulya wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kwa kushirikiana na Wakili wa Serikali Mkuu, Timon Vitalis.
 Mawakili hao, wakiongozwa na Vitalis walidai kuwa  washtakiwa wote watatu katika nyakati tofauti kati ya Septemba Mosi, 2014 na Septemba 30, 2015  katika Mkoa wa Dar es Salaam walikula njama ya kutenda makosa hayo chini ya Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa.
Katika kesi hiyo, ilidaiwa kuwa Februari 27, 2015, Tito katika ofisi za Rahco zilizoko wilayani Ilala, alitumia madaraka yake vibaya kwa kuipitisha kampuni hiyo ya Rothschild kama mshauri wa mradi wa uimarishaji wa Reli ya Kati bila idhini ya Bodi ya zabuni ya Rahco, hivyo kwenda kinyume na Sheria ya Manunuzi ya Umma.
Tito na Massawe  wanadaiwa kuwa Machi 12, 2014 katika ofisi hizo za Rahco walitumia madaraka yao vibaya kwa kutia saini barua rasmi ya kuichagua kampuni hiyo, kama mshauri katika mchakato wa uimarishaji wa njia ya Reli ya Kati kwa kiwango cha kisasa (standard gauge).
Kati ya Machi 12 na Mei 20, 2015 katika ofisi za Rahco, Tito na Massawe wanadaiwa kutumia vibaya madaraka yao kwa kushindwa kuwasilisha mkataba wa huduma ya ushauri, baina ya kampuni hizo mbili kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG).
Pia wanadaiwa kuwa kati ya Mei 20 na Juni 20, 2015 katika ofisi hizo washtakiwa hao, walishindwa kuwasilisha nakala ya mkataba kati ya kampuni hizo kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Mbali na mashtaka hayo, washtakiwa hao kwa pamoja kwa nyakati tofauti kati ya Machi Mosi na Septemba 30, 2015 walitoa huduma ya ushauri kwa kampuni hiyo, bila kufuata taratibu za ununuzi na malipo na walisababisha hasara ya dola za Marekani 527,540 ambazo zililipwa kama  gharama za malipo ya awali.
Agosti 18, 2015, Tito akitekeleza majukumu yake, alitumia vibaya mamlaka kwa kuipatia kampuni ya China Railway Construction Corporation kazi ya ujenzi wa reli kwa kilomita mbili za kiwango cha kisasa kutoka Soga, iliyogharimu dola Marekani 2, 312,229.39 bila ya kuwa na  idhini ya bodi ya zabuni ya Rahco.
Washtakiwa hao hawakuruhusiwa kujibu kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kuisikiliza kesi hiyo hadi Mahakama Kuu.
Uamuzi wa dhamana utatolewa Ijumaa.

Categories: